Wednesday, 16 March 2011

Mrema amfangilia babu wa Loliondo

   
*Akumbusha serikali wajibu wake
Heri Shaaban na Khadija Iddi, Jijini

SIKU chache baada ya Mbunge wa Vunjo kupitia tiketi ya Chama cha Tanzania Labour (TLP), Augustine Mrema kurejea kutoka kunywa dawa ya Mchungaji Mstaafu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Ambilikile Mwaisapile wa Loliondo mkoani Arusha, ameiomba Serikali iwekeze miundombinu ili wananchi waweze kufika bila kikwazo.

Mrema alitoa tamko hilo jana katika wa kipindi cha Usiku wa Habari kinachorushwa na Televisheni ya Taifa (TBC 1) alipokuwa akizungumzia mabadiliko ya afya yake baada ya kutoka kwa mchungaji huyo.

Amesema kuwa kuna haja ya Serikali kuboresha miundombinu ya Loliondo ili kila Mtanzania mwenye matatizo aweze kufika kwa babu kwa kuwa ni mtu mwenye uwezo wa kipekee wa uponyaji.

"Serikali iamue kuwasaida Watanzania wengi kufika kwa babu  kwa kuwa babu ni kama zawadi tuliyoshushiwa kutoka kwa Mungu kuja kuwasadia wale wote wenye magonjwa sugu yaliyo wasumbua kwa muda mrefu," alisema Mrema.

Kwa mujibu wa Mrema, tangu anywe dozi hiyo, ameona mabadiliko ya afya na amesema anachosubiri hivi sasa ni daktari wake aweze kumpima afya na kuelezea bayana kwani amekuwa akisumbuliwa na ugonjwa wa kisukari kwa zaidi ya miaka 35 na watu aliougua nao wengi wamekufa baada ya kukosa tiba sahihi.

Amesema kuwa afya yake itakapoimarika, atahakikisha kuwa anarudi katika majukumu yake ya kila siku na kuwashukuru wananchi wake kwa kumshauri kwenda kutibiwa.

No comments:

Post a Comment