Jamhuri ya Watu wa Zanzibar irejeshwe

SERIKALI ya Mapinduzi Zanzibar leo imesema
kuwa matumizi ya neno Jamhuri ya Watu wa Zanzibar inawezekana ikiwa wazanzibari wengi watatoa maoni ya kulirejesha jina hilo. Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Sheria na Katiba, Abubakar Khamis Bakari wakati akijibu suali la msingi la Mwakilishi wa Jimbo la Mji Mkongwe (CUF) Ismail Jussa Landu aliyetaka kujua kwa nini jina hilo la Jamhuri ya Watu wa Zanzibar lilifutwa.
Jussa aliuliza “Lini serikali ya Zanzibar itarudisha matumizi ya jina la jamhuri na kuyaweka mapinduzi ya Zanzibar katiak misingi yake iliyokusudiwa na Marehemu Mzee Abeid Amani Karume?” alihoji.
Waziri Bakari alisema jina la jamhuri lilikuwa likitumika katiak sheria ya katiba ya zanzibar nambari 5 ya mwaka 1964 kama ilivyotamka sheria namba moja ya mwaka 1964 lakini baada ya kufanyika muungano jamhuri ya watu wa zanzibar ikatoweka.
“Baada ya kufanyika muungano wa tanganyika na jamhuri ya watu wa zanzibar Aprili 26 mwaka 1964 na kuundwa kwa Tanzania matumizi ya jamhuri yalififia na kufutika” alisema Waziri.
Aidha alisema jina la jamhuri ya watu wa zanzibar lilifutika kutokana na sheria na katiba zilizokuwa zikitumika na kuacha kutumia jina hilo baada yake kubuni maneno ya Tanzania bara na Tanzania visiwani.
“ Kisheria jamhuri ya watu wa Zanzibar haikufutwa bali ilikuwa haitumiki na tanzania imekuwa ikitumika kwa muda mrefu bila malalamiko yoyote kwa maana hiyo basi matumizi ya Tanzania ni halali kwa sababu kisheria jina likitumika kwa muda mrefu inakuwa halali” alisema.
Waziri huyo alisema kwa sababu jina halikufutwa kisheria ni rahisi kulirejesha tena pale wazanzibari watakapoamua kulirejesha tena kwa hiyo ni jukumu la wananchi wenyewe wa Zanzibar kuamua na serikali itaheshimu maamuzi yao.
“Kwa kupitia wajumbe wa baraza la wawakilishi kazi ya kutafuta maoni kutoka kwa wananchi wao inaweza kuwa ni rahisi juu ya matumizi ya jina la jamhuri lakini pia nafasi iliyopo juu ya machakato wa maoni ya katiba ya jamhuri ya muungano wananchi wende muyaseme mnayoyataka na maamuzi yenu yataheshimiwa” aliahidi waziri huyo.
MIMI SIO UAMSHO – MANSOOR

WAZIRI wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Mansoor Yussuf Himid amekanusha kuwa yeye si Uamsho na wala hawaungi mkono kama inavyodaiwa mitaani licha ya kukubaliana na kauili mbiu yao.
“Mimi sio Uamsho wala siwaungi mkono nataka kusema wazi hapa maana kuna watu kazi yao kusingizia wenzao, lakini kwa hili la tuachiwe tupumuwe mie nakubaliana nao kwa maana kaulimbiu hii nakubaliana nayo, lakini sio vurugu zao” Alisema Waziri Himid.
Himid ambaye ni waziri asiye wizara maalumu alisema baadhi ya kauli mbinu zinazotilewa na Jumuiya ya Uamsho na Mihadhara ya Kiislamu Zanzibar (JUMIKI) ikiwemo kauli mbiu yao maarufu ya “Tuachiwe Tupumuwe”. Anakubaliana nayo.
Kauli hiyo ameitoa katika kikao cha Baraza la Wawakilishi jana alipokuwa akichangia bajeti ya serikali ya mwaka wa fedha wa 2012/2013.
Alisema hakubaliani kabisa na Jumuiya ya Uamsho na wala yeye haungi mkono mitazamo yao na ametumia fursa hiyo pia kukanusha kwamba hahusiki nayo ingawa wapo baadhi ya watu wanafikiri hivyo kutokana na kukaa kwake kimya kwa muda mrefu.
Waziri Himid ambaye ni muweka hazina wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar amekuwa akisema wazi misimamo yake juu ya Muungano ambapo husema Muungano una matatizo na kuna kila sababu ya kushughulikiwa lakini sio kuuvunja.
“Mheshimiwa Naibu Spika, maoni ya makundi haya yote yanaheshimiwa, lakini katika hili la kuvunjua Muungano sikubaliani na kundi hilo na tutaendelea kuwasihi wakubaliane na sisi katika kudumisha Muungano wetu maana kitu tulichokiunda na kudumu kwa miaka 48 sio jambo la busara na rahisi tuseme tukivunje” Alisema Himid.
Akizungumzia umuhimu wa kuungana alisema kwamba dunia ya leo ni ya watu kuungana Mataifa ya Ulaya yanazidi kuungana, lakini hata Afrika hivyo sio jambo la busara kufikiria kuvunja Muungano.
Katika hatua nyengine amewakosoa baadhi ya watu wanaowataka Wawakilishi kutowasemea Wazanzibari katika madai ya Muungano kuwa wamepotoka na kitendo hicho hakikubaliki katika dhana nzima ya Uwakilishi wa wananchi.
Waziri Himid alisema ni haki ya kila mzanzibari kuzungumzia Muungano na ni dhambi kubwa kwa mtu yeyote kuwakataza Wazanzibari au Watanganyika kuzungumzia Muungano.
Alisema wao ni Wawakilishi wa wananchi ambao wamechaguliwa kuwawakilishi katika chombo cha kutunga sheria hivyo sio sahihi kutokea mtu au kikundi kikadai hawawezi kuwasemea wananchi wote.
“Mimi nasema sio sahihi kusema Wawakilishi wasiwasemee Wazanzibari maana wametuchagua tuwawakilishi humu ndani sas inakuwaje tena tusiseme..mimi nadhani sio sahihi hata kidogo, katika hili hatuwezi kuwazuia watu kusema kuhusu mfumo wa Muungano wanaoutaka.
Waziri huyo alisema ni lazima kuwepo kwa mfumo wa Muungano wenye tija ambao hautaleta malalamiko kwa kila upande. “Muungano ulio sawa na haki” Alisisitiza Waziri huyo.
Alisema kwamba msingi wa Muungano ni mkataba na sio katiba ambapo ikiwa kutakuwa na mfumo bora na wenye tija Zanzibar itakuweza kuwa mwanachama wa Umoja wa Mataifa, kujiunga na mshirika mbalimbali ya Kimataifa akiyataja kwa uchache kama FAO,FIFA, Benki ya Dunia, UNFPA, WHO na mengineyo.
“Tukiwa na mfumo mzuri ambao utaifanya Zanzibar kuwa na kiti chetu UN, tuweze kujiunga na Jumuiya za Kimataifa tutakuwa tumeweka msingi mzuri katika Muungano wetu.
Waziri Himid aliwanasihi wazanzibari kutokubali kuondoshwa kwenye malengo yao kuhusu suala zima la Muungano na umuhimu wa kila mtu kutoa maoni yake wakati Tume ya Katiba itakapoanza kuchukua maoni ya wananchi hapa nchini.
“Nawaombeni wananchi wenzangu itakapofika Tume ya Mheshimiwa Jaji Warioba twendeni tukatoe maoni yetu na wala tusikubali kupoteza malengo yetu kwa sababu ya mtu au kikundi fulani, kwani umoja ni nguvu na utengano ni udhaifu” Alisema Waziri huyo.
Waziri Himid alisema katika harakati za kuelekea mchakato wa katiba mpya ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kumekuwepo na kaulimbiu miongoni mwa wananchi ya “Tuachiwe tupumuwe” ambayo imeasisiwa na Uamsho katika madai ya kuidai Zanzibar huru.
BALOZI NDOGO ZANZIBAR

SERIKALI ya Zanzibar inapendelea kuona nchi mbali mbali zilizopo na ubalozi hapa Tanzania zinafungua balozi ndogo upande wa Zanzibar ili kuimarisha mahusiano mema.
Hayo yameelezwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamo wa Pili wa Rais, Mohammed Aboud Mohammed akijibu suali la Mwakilishi wa Jimbo la Amani (CCM) Fatma Mbarouk Said aliyetaka kujua ni nchi ngapi zimefungua ofisi yake Zanzibar.
Waziri Aboud alisema serikali inaendelea na itaendelea kuwasiliana na ofisi mbali mbali za kibalozi zilizopo Dar es salaam ili zifungue ofisi zao Zanzibar.
“Tunataka ofisi za kibalozi zilizopo Dar es salaam ziwepo na Zanzibar ili kuimarisha zaidi mahusiano” alisema Waziri huyo.
Akizitaja nchi tano zenye ofisi za kibalozi ndogo Zanzibar mbele ya wajumbe wa baraza la wawakilishi, ni China, India, Misri, Msumbiji na Oman ambazo zina ofisi zake hapa Zanzibar.
Aidha alitaja Uingereza, Sweden Norway na Denmark kuwa zina mabalozi wa heshima wenye makaazi yao hapa Zanzibar.
UPUNGUFU WA WATAALAMU KATIKA HALMASHAURI

WAZIRI wa Nchi ofisi ya rais Dk Mwinyihaji Makame Mwadini amesema upo upungufu wa watendaji na wataalamu katika halmashauri mbali mbali Unguja na Pemba.
Akijibu suali la Mwakilishi wa Jimbo la Mtambile (CUF) Mohammed Haji Khalid aliyekaa kujua juhudi za serikali katika kuimarisha juhudi za utendaji kwenye hamlashauri ya chakechake Pemba. Dk Mwinyihaji alisema serikali inaweka mikakati ya kuimarisha serikali za mitaa.
“serikali katika kulitatua tatizo hili tayari imetayarisha sera ya serikali za mitaa na imeweka mikakati maalumu ya kuongeza wataalamu wa aina mbali mbali” alisema Dk Mwinyihaji.
Waziri huyo alisema wizara yake imewasilisha maombi maalumu katika ofisi ya utumishi wa umma kwa ajili ya kupata wataalamu na kuondosha tatizo la upungufu wa nguvu kazi katika halmashauri zote za Unguja na Pemba.
Alisema katika mpango huo wanasheria wataajiriwa pamoja na wahasibu ili kuimarisha ukusanyaji wa mapato madogo madogo katika halmashauri hizo na kuimarisha serikali za mitaa.
Zanzibar ina wilaya 10 na halmashauri kadhaa ambapo wajumbe wa baraza la wawakilishi wamekuwa wakilalamikia kutokuwepo na utaratibu mzuri wa ukusanyaji wa mapato.
UWAJIBIKAJI SERIKALINI NI HABA

KUTOKUWEPO kwa ufanisi wa kazi katika baadhi ya taasisi za serikali ya zanzibar kunatokana na tabia ya utoro.
Kauli hiyo imetolewa ndani ya kikao cha baraza la wawakilishi kinachoendelea hapa Zanzibar na waziri wa nchi ofisi ya rais utumishi wa umma na utawala bora, Haji Omar Kheri wakati akijibu suali la Mwakilishi wa Jimbo la Muyuni (CCM) Jaku Hashim Ayoub.
Ayoub alitaka kujua sababu zinazopelekea watendaji wakuu kushindwa kusimamia majukumu yao na kuruhusu tatizo la utoro na uvivu kuendelea katika maeneo ya kazi.
Waziri Kheri alisema “Tatizo la uvuvi, utoro ruhusa za harusi, maulidi na mazikoni ni mambo ambayo hupunguza ufanisi wa kazi na kupoteza muda mwingi kazini. Hii inatokana na kutosimamiwa ipasavyo” alisema waziri.
Waziri alilaumu baadhi ya watendaji katika taasisi za serikali kwa kushindwa kusimamia majukumu yao kutokana na tabia ya muhali.
“Kwa kuwa tabia hii ya muhali imejengekea kwa miaka mingi sio rahisi kuondosha mara moja hata hivyo kila mmoja wetu kwa pale alipo lazima atekeleze wajibu wake ipasavyo kwa mujibu wa sheria” alisema.
Mwakilishi wa Jimbo la Magomeni (CCM) Salmin Awadh Salmin alitaka kujua mipango iliyopo ya kuondosha tatizo la muhali katika sehemu za kazi ambapo waziri alijibu kuwa kuna utaratibu maalumu umeanzishwa kuwapima watendaji.
Waziri Kheri alisema zipo sheria za umma pamoja na sera ambazo zinatoa adabu kwa uvivu, utoro na asiyewajibika na kutaka watendaji watumie sheria hizo ili kuimarisha ufanisi.
“Kwa sasa kila wizara ina mpango kazi wa robo mwaka na kila mtumishi hupangiwa majukumu ya kufanya kwa kila siku ipo pia suala zima la kutathimini watendaji kwa kutumia fomu maalumu ya upimaji, utendaji wa wafanyakazi, haya yatasaidia kuondosha muhali” alisema waziri huyo.
No comments:
Post a Comment