Na Talib Ussi Zanzibar
KATIBU Mkuu wa Chama cha Wananchi CUF ambaye piya ni Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Maalim Seif Sharif Hamad amesema viongozi wa serikali za mitaa (Masheha) wanawanyima fomu za kuombea vitambulisho vya Mzanzibari Mkaazi wafuasi wa CUF kwa makusudi ili kinapoteza nguvu ya ushindi katika uchaguzi mkuu ujao.
Malim Seif aliyasema hayo leo ( jana) wakati akihutubia kwenye sherehe zilizoandaliwa na jimbo la Mtoni kuadhimisha mwaka mmoja wa ushindi wa chama hicho katika jimbo hilo zilizofanyika Bwawani mjini Zanzibar.
Alisema Masheha wanawanyima fomu wananchi hao kwa makusudi baada ya kupokea maagizo kutoka kwa viongozi wasioitakia mema Zanzibar na ambao wanachukizwa na hali ya amani na utulivu inayoendelea kudumu Zanzibar, tokea kufikiwa maridhiano ya kisiasa Novemba 2009.
Alielekeza Masheha wenye tabia hiyo wanapaswa kuiacha mara moja kwasababu vitambulisho vya Mzanzibari Mkaazi mbali na kutumika kwenye kura, lakini pia vinatumiwa na wananchi kupata huduma muhimu na kwa mujibu wa sheria.
“Masheha hawa wanaowazuia Wazanzibari wasipate vitambulisho hivyo wanatenda makosa” aliseam Maalim Seif.
“Mheshimiwa Rais kama hujui hili nakwambia, tumevumilia mwaka mzima, leo hii tumefikia hatua anatokea kiongozi wa CCM kutoka Bara anatoa maelekezo kama hayo kwa Masheha”, aliendelea kwa kulalamika Maalim Seif.
Alisema kwamba viongozi wa CUF kuwemo ndani ya serikali haimaanishi kuwa wakae kimya.,
“Vitambulisho vya ukaazi ni haki ya kila Mzanzibari aliyefikia umri wa miaka 18 ni haki yake ya kidemokrasia ambayo viongozi wote wa CCM na CUF wameahidi watailinda katika utekelezaji wa majukumu yao” alifahamisha katibu Mkuu huyo wa CUF.
Katibu Mkuu wa CUF alisema hali hiyo inasikitisha hasa kuona wananchi wanaokoseshwa vitambulisho hivyo ni wa upande mmoja tu na wale wa CCM wote wanapatiwa vitambulishi vya ukaazi mara wanapovihitaji.
Alieleza kwamba anahaki ya kuwashitua viongozi wenye tabia hiyo kwa sababu kuja kwa serikali ya umoja wa kitaifa Zanzibar hakumaanishi vyama vya siasa havipo tena.
“Vyama hivyo vipo pale pale kila kimoja kikitekeleza majukumu yake” alikemea Malim Seif.
Akizungumzia suala la Katiba mpya, Maalim Seif ambaye pia ni Makamo wa Rais wa Zanzibar aliwataka wafuasi wa CUF na wananchi wote wa Zanzibar kujiweka tayari kwa ajili ya kuchangia mjadala huo.
Alisema baada ya Bunge kipitisha mswada wa marekebisho hayo ambayo huenda utawasilishwa Bungeni katika vikao vya hivi karibuni.
Alisema kuhusu suala la mfumo wa Muungano, sera ya chama cha Wananchi CUF iko wazi juu ya hilo, ambapo chama hicho kinataka mfumo wa Muungano wa serikali tatu, kama njia muafaka ya kumaliza migogoro mingi inayojitokeza ndani ya Muungano huo .
“Naamini Bunge linalokuja mswada wa marekebisho ya Katiba utafikishwa naomba waheshimiwa tutumie nafasi vizuri , wana CUF tunajua sera ya chama chetu inataka mfumo wa serikali tatu kuondoa malalamiko ndani ya Muungano”, alisema Maalim Seif.
Katika mkutano huo, Mwakilishi wa jimbo la Mtoni ambaye ni Waziri wa Biashara na Viwanda, Nassor Ahmed Mazrui alisema hadi sasa wamefanikiwa vizuri kutekeleza ahadi walizozitoa kwa wananchi wakati walipokuwa wakiwaomba kura kabla ya uchaguzi mkuu uliopita.
Waziri Mazrui alisema katika kuhakikisha huduma muhimu za kijamii zinawafikia wananchi wa jimbo hilo, ikiwemo maji safi na salama yeye binafsi hadi sasa ameshatumia shilingi milioni 280, ikiwemo kufanikisha ujenzi wa visima vya maji tisa, kufanikisha upasuaji kwa akinamama wenye matatizo, pamoja na kuhudumia mazishi na elimu
No comments:
Post a Comment