Watu wangu wananipenda- Gaddafi
Kiongozi wa Libya Kanali Muammar Gaddafi ameiambia BBC kuwa anapendwa na watu wake wote, na amekanusha kuwa kuna maandamano yanafanyika mjini Tripoli.

Muammar Gaddafi
Kanali Gaddafi amesema watu wake wako tayari kufa kwa ajili ya kumlinda.
Ametupilia mbali taarifa kuwa ataondoka Libya, na kusema anahisi kusalitiwa na viongozi wanaomtaka aondoke madarakani.
Aondoke sasa
Mapema, serikali za nchi mbalimbali duniani zililaani mashambulizi dhidi ya raia wa Libya, huku waziri wa mambo ya nje wa Marekani Hillary Clinton akisema Kanali Gaddafi lazima "aondoke sasa".Umoja wa Ulaya siku ya Jumatatu uliweka vikwazo vya silaha, kupiga tanji na kuweka vikwazo vya kusafiri kwa Kanali Gaddafi na washirika wake.

Askari wanaompinga Gaddafi
Kanali gaddafi alikuwa akizugumza katika mahojiano na mwandishi wa BBC Jeremy Bowen mjini Tripoli.
Kanali Gaddafi amesema watu waliojitokeza mitaani kuandamana, walikuwa wamelewa baada ya kupewa ulevi na al-Qaeda.
Risasi
Amesema watu hao walipora silaha na kuwa wafuasi wake wana amri ya kutopiga risasi.Mwandishi wetu anasema Kanali Gaddafi alikuwa katika hali ya utulivu wakati wa mahojiano hayo kwenye mgahawa ulio karibu na bandari ya Tripoli. Muda mfupi baadaye aliondoka kwa kasi katika msafara wa zaidi ya magari kumi.

Muammar Gaddafi
Kanali Gaddafi, anakabiliwa na changamoto kubwa katika utawala wake wa miaka 41, kwa waandamanaji kudhibiti miji ya mashariki.
Ghasia pia zinaendelea ndani na kuzunguka mji wa Tripoli, huku taarifa za waandamanaji wanaompinga Gaddafi zikiwepo katika viunga vya mji mkuu na mji wa karibu wa Misrata. Pia kuna taarifa za shambulio kwa njia ya anga katika eneo la kutupia silaha kukuu mashariki mwa nchi.

Hillary Clinton akizungumza katika kikao cha Geneva
Awali mawaziri wa mambo ya nje waliokutana katika mkutano wa Umoja wa Mataifa mjini Geneva wametoa wito kwa kanali Gaddafi kuondoka.
Waziri wa mambo ya nje wa Marekani, Hillary Clinton amemtuhumu Kanali Gaddafi wa wafuasi wake kwa kutumia "mamluki na wahuni" kushambulia raia wasio na silaha, na kuua wanajeshi wanaokataa kuwashambulia raia.
No comments:
Post a Comment