Mamilioni yatumika kulipia mawaziri mahoteli


Serikali inatumia mamilioni ya fedha kwa ajili ya kuwapangishia hoteli baadhi ya mawaziri wapya na manaibu wake baada ya kukosa nyumba za kuishi huku wale wa zamani wakiendelea kumiliki nyumba hizo.
Uchunguzi wa gazeti hili umebaini kwamba baadhi ya viongozi hao wamepangishiwa nyumba za gharama (apartment), kwenye hoteli kubwa jijini Dar es Salaam.
Hoteli hizo ni pamoja na Ubungo Plaza, Ubungo, New Africa Hotel, katikati ya Jiji na Protea Courtyard eneo la Sea View.
Baadhi ya viwango vinavyolipwa katika hoteli hizo Ubungo Plaza ni dola za Marekani 105 kwa siku na Protea ambako kwa siku ni kati ya dola za Marekani 155 na 180.
Mawaziri hao walianza kuishi kwenye hoteli hizo tangu walipoapishwa rasmi kushika nyadhifa zao katikati ya mwezi Novemba, mwaka jana.
Uchunguzi zaidi unaonyesha kwamba chakula katika hoteli ya Protea ni dola 20 kwa sahani wakati Ubungo Plaza, gharama ya pango inajumuisha na mlo mmoja.
Hata hivyo, sababu za kukosa nyumba haziwekwi bayana wakati takwimu zinaonyesha kwamba katika Baraza la Mawaziri lililopita, Naibu Mawaziri walikuwa 21 na sasa idadi ni hiyo hiyo.
Waziri wa Fedha na Uchumi, Mustafa Mkulo, alipotafutwa kuelezea gharama zinazotumika kuwalipia viongozi hao, alisema asingependa kulizungumzia suala hilo kwa kuwa kuna Wizara husika ambayo ingetakiwa kujibu masuala hayo.
"Kwa kweli mwandishi suala hilo nikilizungumzia nitaonekana nimeingilia masuala ya wizara nyingine hivyo nakuagiza uende kwa katibu Mkuu wa Miundombinu Omari Chambo atakueleza au ukimkosa hata Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais ( Menejimenti ya Utumishi wa Umma) Hawa Ghasia atalizungumzia suala hilo ila kwa mimi nitakuwa nimeingilia wizara," alisema Mkulo
Hata hivyo, Chambo alipoulizwa juu ya suala hilo alisema hawezi kuzungumza suala hilo kwenye simu na kutaka afuatwe ofisini kwake na kuamua kukata simu.
Baada ya mazungumzo hayo Nipashe Jumapili ilifika ofisini kwa Chambo, lakini mwandishi alitakiwa kuacha maswali kwa Katibu Muhtasi.
Waziri wa Ujenzi, John Magufuli naye alipotafutwa ili kutoa ufafanuzi wa suala hilo hakuweza kupatikana kutokana na kuwa na majukumu mbalimbali ambapo hata simu yake ilikuwa inaita bila kupokelewa.
Habari za ndani kutoka katika ofisi ya Wizara ya Ujenzi zimedai kuwa mawaziri wa zamani ambao bado wanaishi kwenye nyumba hizo za serikali wameshapewa notisi ya kuondoka haraka.
Taarifa za kupewa notisi kwa mawaziri hao wa zamani zilitolewa na chanzo chetu cha habari ndani ya wizara hiyo ambacho kilisisitiza kuwa sababu ya mawaziri wa sasa kupangishiwa hoteli ni kutokana na ukosefu wa nyumba.
Chanzo hicho kilidai kuwa mchakato uliopo ni kwamba tayari mawaziri wameshaambiwa waondoke mpaka ifikapo wiki ijayo wawe wameziachia nyumba hizo.
"Mawazi hao tayari wameshapatiwa muda mpaka wiki ijayo wawe wameshaondoka ili mawaziri waliopangishiwa hotelini waweze kuishi katika nyumba hizo za serikali," alisema.
Chanzo hicho kiliendelea kudai kuwa serikali inatumia gharama kubwa kuwalipia mawaziri hao kutokana na kupangishiwa hoteli kubwa.
"Unajua hawa mawaziri hawawezi kuwekwa katika hoteli za maeneo ya Kariakoo au Sinza kutokana na usalama wao na ndio maana tumewatafutia katika hoteli hizo," kilidai chanzo hicho.
Aidha, serikali imeamua kutoa muda kwa mawaziri hao kutoka katika nyumba hizo za serikali ili kupunguza gharama zinazotolewa.
No comments:
Post a Comment