Thursday, 17 March 2011

CCM kujitathimini mwezi ujao
Sadick Mtulya
HALMASHAURI  Kuu ya Taifa ya CCM,  inatarajiwa kukutana  mjini Dodoma mwezi ujao, kupitia na kutathmini taarifa kuhusu mambo yaliosababisha chama hicho, kushindwa katia baadhi ya maeneo katika uchaguzi mkuu  uliopita.

Hatua hiyo inafuatia agizo lililotolewa mwishoni mwa mwaka jana na Mwenyekiti wa CCM Rais Jakaya Kikwete, wakati alipokutana na Jumuiya wa Wanawake wa ya CCM (UWT), katika viwanja vya Biafra jijini, Dar es Salaam.

Jana, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, John Chiligati, aliiambia Mwananchi kuwa kikao hicho pia kitajadili mambo mbalimbali ya chama na mustakabali wake.

"Pamoja na mambo mengine Nec,itapitia na kutathmini  ripoti  ya mambo yaliosababisha chama kushindwa kwenye baadhi ya maeneo katika uchaguzi mkuu  uliopita,"alisema Chiligati.Chiligati alisema hatua hiyo imetokana na  kukamilika kwa ripoti za tathimini ya uchaguzi, zilizofanywa na viongozi wa CCM kote nchini.

Hata hivyo, Chiligati hakuwa tayari  kutaja ajenda nyingine zitakazojadiliwa katika kikao hicho.Lakini kwa mujibu wa chanzo chetu, kikao hicho pia kitafanya kazi ya kupitisha majina ya viongozi  wapya wa chama katika ngazi zote.

"Ingawa nafasi ya katibu mkuu inapendekezwa  na  mwenyekiti wa chama, lakini  baadhi ya wananchama wameonyesha nia ya kuitaka nafasi  hiyo pamoja na nyingine," kilisema chanzo hicho.

Kwa sasa nafasi ya Katibu Mkuu wa CCM inashikiliwa na Yusufu Makamba, ambaye hata hivyo amekuwa akituhumiwa kwa kushindwa kukiendesha vema.

Desemba 5 mwaka  jana, Rais Kikwete aliwataka wanachama na viongozi wa chama hicho katika ngazi zote, kuangalia kwa makini mambo ambayo yalisababisha chama hicho kushindwa kwenye baadhi ya maeneo katika uchaguzi mkuu.

"Shabaha yetu ni kuimarisha yale tuliyofanya vizuri, tufanye tathmini hii mapema ndani ya miezi hii mitatu au sita iwe imekamilika, tufanye tathimini katika ngazi zote, tukikamilisha tutajua wapi tumekosea wapi tumefanya vizuri, kwenye uchaguzi mkuu ujao tutaingia tukiwa na uhakika," alisema  Rais Kikwete.

Rais Kikwete pia aliwataka viongozi wa UWT, kuwashawishi vijana na wasomi kujiunga na  jumuiya hiyo ili kuzidi kukiimarisha chama hicho. Alisema juhudi za wanawake ndizo zilizokisaidia chama hicho kuibuka na ushindi, huku akiwaelezea  walikuwa wakijitokeza kwa wingi katika mikutano ya kampeni pamoja  na siku ya kupiga kura.

"Mnaotakiwa kupongezwa ni nyie, kupitia nyie hata wanaume na vijana waliipigia kura CCM," alisema Kikwete.Alisema serikali yake itaendelea kutoa nafasi za juu kwa wanawake, ili kutimiza lengo la usawa kitu ambacho ameeleza kuwa ni sera ya CCM.

No comments:

Post a Comment