Sadick Mtulya
HALMASHAURI Kuu ya Taifa ya CCM, inatarajiwa kukutana mjini Dodoma mwezi ujao, kupitia na kutathmini taarifa kuhusu mambo yaliosababisha chama hicho, kushindwa katia baadhi ya maeneo katika uchaguzi mkuu uliopita.
Hatua hiyo inafuatia agizo lililotolewa mwishoni mwa mwaka jana na Mwenyekiti wa CCM Rais Jakaya Kikwete, wakati alipokutana na Jumuiya wa Wanawake wa ya CCM (UWT), katika viwanja vya Biafra jijini, Dar es Salaam.
Jana, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, John Chiligati, aliiambia Mwananchi kuwa kikao hicho pia kitajadili mambo mbalimbali ya chama na mustakabali wake.
"Pamoja na mambo mengine Nec,itapitia na kutathmini ripoti ya mambo yaliosababisha chama kushindwa kwenye baadhi ya maeneo katika uchaguzi mkuu uliopita,"alisema Chiligati.Chiligati alisema hatua hiyo imetokana na kukamilika kwa ripoti za tathimini ya uchaguzi, zilizofanywa na viongozi wa CCM kote nchini.
Hata hivyo, Chiligati hakuwa tayari kutaja ajenda nyingine zitakazojadiliwa katika kikao hicho.Lakini kwa mujibu wa chanzo chetu, kikao hicho pia kitafanya kazi ya kupitisha majina ya viongozi wapya wa chama katika ngazi zote.
"Ingawa nafasi ya katibu mkuu inapendekezwa na mwenyekiti wa chama, lakini baadhi ya wananchama wameonyesha nia ya kuitaka nafasi hiyo pamoja na nyingine," kilisema chanzo hicho.
Kwa sasa nafasi ya Katibu Mkuu wa CCM inashikiliwa na Yusufu Makamba, ambaye hata hivyo amekuwa akituhumiwa kwa kushindwa kukiendesha vema.
Desemba 5 mwaka jana, Rais Kikwete aliwataka wanachama na viongozi wa chama hicho katika ngazi zote, kuangalia kwa makini mambo ambayo yalisababisha chama hicho kushindwa kwenye baadhi ya maeneo katika uchaguzi mkuu.
"Shabaha yetu ni kuimarisha yale tuliyofanya vizuri, tufanye tathmini hii mapema ndani ya miezi hii mitatu au sita iwe imekamilika, tufanye tathimini katika ngazi zote, tukikamilisha tutajua wapi tumekosea wapi tumefanya vizuri, kwenye uchaguzi mkuu ujao tutaingia tukiwa na uhakika," alisema Rais Kikwete.
Rais Kikwete pia aliwataka viongozi wa UWT, kuwashawishi vijana na wasomi kujiunga na jumuiya hiyo ili kuzidi kukiimarisha chama hicho. Alisema juhudi za wanawake ndizo zilizokisaidia chama hicho kuibuka na ushindi, huku akiwaelezea walikuwa wakijitokeza kwa wingi katika mikutano ya kampeni pamoja na siku ya kupiga kura.
"Mnaotakiwa kupongezwa ni nyie, kupitia nyie hata wanaume na vijana waliipigia kura CCM," alisema Kikwete.Alisema serikali yake itaendelea kutoa nafasi za juu kwa wanawake, ili kutimiza lengo la usawa kitu ambacho ameeleza kuwa ni sera ya CCM. |
No comments:
Post a Comment